Kwa nini baadhi ya watoto hukata uhusiano na wazazi wao?

Chanzo cha picha, FreePik
- Author, Miriam Frankel
- Nafasi, BBC
Wataalamu wanasema suala la familia kutengana linaongezeka katika miaka ya sasa.
Utafiti mmoja uliochapishwa mwaka 2022 kwa kuwahoji watu 8,500 nchini Marekani ulibaini kuwa 26% kati yao walikuwa na vipindi vya kutengana na baba zao na 6% kutengana na mama zao katika kipindi cha miaka 24.
Utafiti kama huo wa watu 10,200 nchini Ujerumani uligundua 9% ya wale walijibu kuwa walitengana na mama zao na 20% walitengana na baba zao katika kipindi cha miaka 13.
Katika uchunguzi mwingine huko Marekani wa watu 1,340 ulioelezwa kwa kina katika kitabu kilichochapishwa 2020, mwanasosholojia Karl Pillemer wa Chuo Kikuu cha Cornell anasema aligundua 10% ya watu kwa sasa wametengana kabisa na mzazi au mtoto - bila mawasiliano yoyote.
"Katika vizazi vya kabla ya vita vya pili vya dunia, kulikuwa na kanuni ya mshikamano wa familia - kwamba damu ni nzito kuliko maji. Kanuni hizo zimedhoofika," anasema Pillemer.
Nini chanzo?

Chanzo cha picha, Getty Images
“Kanuni mpya za kifamilia, kama vile wapenzi wanaoishi pamoja bila ndoa na wanandoa wasio na watoto zimeenea zaidi,” anasema Pillermer.
Joshua Coleman, mwanasaikolojia anaefanya kazi na familia zilizotengana na ambaye ameandika vitabu kadhaa juu ya mada hiyo, anasema, kuongezeka kwa ubinafsi kunaweza pia kusababisha utengano.
"Utamaduni wa ubinafsi ni mtu kujishughulisha na yeye mwenyewe tu, furaha yake mwenyewe," anasema. "Na kwa hivyo uhusiano wetu na watu wengine linakuwa ni kama jambo la ziada."
Uchunguzi unaonyesha wazazi watu wazima nchini Marekani wana uwezekano wa kuwa na uhusiano mbaya na watoto wao zaidi ya mara mbili kuliko wazazi katika nchi kama vile Israel, Ujerumani na Uingereza.
Coleman anadai jambo hili linachangiwa zaidi na mitandao ya kijamii. Ni rahisi kupata marafiki katika moja ya mtandao, na watu wengi wenye ushawishi au washauri nasaha wanatuhimiza kukata uhusiano na watu wenye mahusiano mabaya na sisi.
Lakini haimaanishi kwamba kukata mahusiano ni uamuzi mbaya. Watu wengi wana sababu nzuri za kufanya hivyo, hasa wale ambao wamepitia mateso mabaya utotoni, anasema Pillemer.
"Kusiwe na unyanyapaa wa kijamii kuhusu jambo hilo," anasema Coleman, aongeza kwamba huenda wazazi wana tabia mbaya.
Lakini Pillemer anasema utafiti wake, ambao ulijumuisha mahojiano ya kina na watu 300 waliotengana, uligundua kuwa mara nyingi ni "kutokana na mivutano midogo midog,” kama vile mivutano na wakwe, mzazi wa kambo, mahusiano ya jinsia moja, talaka - ni mambo ambayo husababisha mtu kukata uhusiano.
Katika utafiti wa Lucy Blake, mhadhiri wa saikolojia katika Chuo Kikuu cha Magharibi mwa Uingereza na mwandishi wa kitabu cha No Family is Perfect, watu wapatao 800 nchini Uingereza, wengi walitaja unyanyasaji wa kihisia kama sababu. Kama vile wazazi kuwa wakali, kudhibiti watoto au kutumia nguvu.
"Sidhani kama kuna ulazima mtu abaki kwenye uhusiano ambao hajisikii salama," anasema. "Mara nyingi, tunafikiria unyanyasaji wa kimwili au wa kijinsia, lakini unyanyasaji wa kihisia ni muhimu kuuzingantia pia."
Kuwatendea haki wazazi

Chanzo cha picha, Getty Images
Coleman na Pillemer wanasema unyanyasaji wa kihisia ni neno tata ambalo linaweza kutumika vibaya. Wakati mwingine mtoto anaweza kuwa na ugonjwa wa akili au tatizo la matumizi ya dawa za kulevya ambalo linamfanya kuwaona wazazi ni maadui kwa kutomuunga mkono.
Mwanafalsafa Christopher Cowley kutoka Chuo Kikuu cha Dublin, alipoulizwa ikiwa ni lazima watoto wawe na na uhusiano wa kudumu na wazazi. "Kwa upande mmoja, nina deni kwa wazazi wangu kwa kila kitu walichonifanyia," anasema.
“Lakini ikiwa napitia unyanyasaji mbaya kutoka kwa wazazi, basi nitakuwa sina deni nao. Uhusiano bora kati ya mzazi na mtoto mtu mzima," anasema, "unapaswa kuwa wa kirafiki.”
Tunapokuwa watoto wajibu unakuwa kwa wazazi wetu. Lakini hilo linabadilika kadiri tunavyozeeka. Mabaro baro hutaka kuwalaumu wazazi wao kwa kila kitu. Lakini ukishakuwa mtu mzima huwezi kulaumu matatizo yako yote kwa wazazi wako.”
Anasema, kuna wakati fulani, wazazi wetu wanakuwa wazee na dhaifu. Hapo tunatakiwa, kuonyesha subira na rehema zaidi kwao.
Kwa hivyo, ikiwa tunataka kuwatendea haki wazazi wetu, tunapaswa kuzingatia hali zao pia. Je, wamefikia umri wa ukosefu wa maarifa, ugonjwa wa akili, kiwewe au hali duni ya kifedha – hayo yote yanaweza kuchangia matatizo.
Coleman, anasema wakati mwingine kuna mtoto ambaye amelelewa na mama mmoja bila msaada wowote wa baba. Mtoto husema, 'ulikuwa unakwenda sana kazini na nilijihisi kutelekezwa."
"Na kwa upande mmoja, mzazi anapaswa kuwa na huruma na hilo. Lakini mtoto anapaswa pia kuwa na huruma kwamba alikuwa anafanya kazi ili kumleta."
Kujaribu kuelewa tabia za wazazi wetu kunaweza kutupa amani ya akili. Inaweza kutufanya tutambue kwamba si yote waliyofanya yalikuwa mabaya au ya makusudi.
Kipi cha kufanya?

Chanzo cha picha, Getty Images
Cowley anapendekeza tukumbuke madhara ya kisaikolojia ya maisha yote ya kutengana kabla mtu hajaamua kujitenga. Kuweka baadhi ya njia za mawasiliano wazi hutoa uwezekano wa mazungumzo kurudi kwa urahisi..
Iwapo tutakata mahusiano milele, huenda tukatumia maisha yetu yote tukihangaika kuelewa kilichotokea. Ni muhimu pia kuwatendea wengine jinsi tunavyotaka kutendewa sisi. Fikiria katika siku zijazo, ungehisije ikiwa mtoto wako mtu mzima atasema malezi yako yalikuwa duni, kulingana na viwango vyake vya kisasa?
Jambo la mwisho la kuzingatia: Je kumbukumbu zako za utoto ni sahihi? Kumbukumbu ya binadamu ina makosa, na mara nyingi huwa tunakumbuka mambo vibaya au kutengeneza kumbukumbu za uongo, hasa tukiwa watu wazima.
“Swali pia, kukata uhusiano kutatufanya tuwe na furaha? Tafiti zinaonyesha watoto mara nyingi wanasema wanahisi furaha zaidi wakikata ihusiano," anasema Coleman. "Ingawa kwa wazazi ni kinyume chake. Ni huzuni na kuchanganyikiwa."
Lakini Blake amegundua kuwa watoto wengi walioachana na wazazi wao wanatatizika, haswa wakati wa likizo. Kwa hivyo, ikiwa una nia ya kukata uhusiano na wazazi wako, jitayarishe kuwa na mtandao wa usaidizi karibu nawe, anashauri.
Cowley anaeleza. "Nadhani jambo hili linadhuru mtoto pale anapopoteza mawasiliano na mahali alipotoka."
Cowley, Pillemer na Coleman wanasema, ikiwa huwezi kustahimili kuwa na uhusiano na wazazi wako, unapaswa kujitenga kwa muda mfupi. Watoto wanaochagua kujitenga warudi kwa wazazi wao baada ya mwaka mmoja. Wakati mwingine, muda huo unatosha kusawazisha mambo."
Upatanisho unawezekana. Utafiti wa 2022 wa watu 8,500 nchini Marekani ulikadiria kuwa 62% ya watu ambao walikuwa wametengana na mama zao na 44% ambao walikuwa wametengana na baba zao walipatanishwa, katika kipindi cha miaka 10.